Wananchi wilayani Nkasi Mkoani Rukwa wamewataka wagombea nafasi za ubunge na udiwani wilayani humo kutimiza ahadi zao kwa wananchi pindi watakapochaguliwa katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 29,2025.

 Wakizungumza  na Ndingala Fm ,leo Septemba 12, 2025 katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika kata ya korongwe  baadhi ya wananchi akiwemo Siwema Mtanga amesema wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge wanapaswa kutekeleza ahadi wanazozitoa katika kampeni hususani changamoto ya miundombinu ya barabarani.

"Ahadi hizi tumezizoea watatue changamoto za miundombinu ya barabara,afya, maji , matibabu bure kwa wa mama wajawazito ,wazee na watoto."amesema Mtanga

Awali akizungumza katika mkutano huo wa kampeni mwenyekiti wa vijana wilaya ya Nkasi Frances maembe amesema matarajio ya wananchi kwa wagombea ni uboreshaji wa miundombinu ya barabara ambayo imekuwa ni kilio cha wananchi kushindwa kufanya shughuli nyingi za usafirishaji wa mazao hasa katika kata hiyo.

Mzee Hamisi Mbalamwezi kutoka kata ya ya Korongwe amesema barabara na huduma za afya imekuwa ni kero kubwa katika kata yao na kumtaka mgombea ubunge katika Jimbo hilo kuitimiza ahadi hiyo kwa vitendo.

"Shughuli yetu kubwa ni uvuvi tunavua na kusafirisha samaki maeneo mbalimbali barabara ni changamoto kubwa hasa nyakati za mvua nimwombe mgombea kuhakikisha akipata nafasi hii atutatulie changamoto hii."amesema Mzee Mbalamwezi 

 Mgombea ubunge  wa jimbo la Nkasi kaskazini Salum Kazukamwe ameahidi kushirikiana na wananchi pamoja na viongozi wa chama na serikali ili ahadi anazozitoa zitekelezeke  kwa vitendo .


"Mkinipa ridhaa Oktoba 29 nitahakikisha nashughulika na changamoto za uhuduma za afya ,shule na kuhakikisha wavuvi wanapata mikopo ili kuachana na uvuvi wa kienyeji." amesema Kazukamwe 

Kazukamwe amesema atahakikisha watu wenye ulemavu,wazee, wanawake na vijana wanapata bima ya afya kwa wote ili kuondokana na changamoto za huduma za afya katika maeneo yao

MWISHO.