Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mheshimiwa Charles Makongoro Nyerere, ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa mchango wake mkubwa katika kuimarisha haki, ustawi wa jamii na maendeleo ya Taifa kwa ujumla, akieleza kuwa Mahakama ni mhimili muhimu unaolinda misingi ya usawa na utawala wa sheria.

Mheshimiwa Makongoro ametoa pongezi hizo alipokuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mkoa wa Rukwa, yaliyofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu ya Tanzania, Masijala ya Sumbawanga. Maadhimisho hayo yaliwakutanisha wadau mbalimbali wa haki na wananchi, yakilenga kutafakari mchango wa Mahakama katika maendeleo ya Taifa.


Akizungumza katika hafla hiyo, Mheshimiwa Makongoro amesema Mahakama ina jukumu la kipekee la kutoa haki kwa wananchi bila upendeleo, akisisitiza kuwa utoaji wa haki kwa weledi na kwa wakati ni msingi wa kudumisha amani na mshikamano katika jamii.

Aidha, Mheshimiwa Makongoro ametoa rai kwa Mahakama kuendelea kusogeza huduma zake karibu zaidi na wananchi kwa kupanua wigo wa utoaji wa huduma, ikiwemo ujenzi wa vituo vya Mahakama kwa kushirikiana na wananchi. Amebainisha kuwa wananchi wa Mkoa wa Rukwa wamekuwa mstari wa mbele katika kuchangia shughuli za maendeleo ya Taifa, hivyo wanastahili huduma za haki zilizo karibu nao.


Mheshimiwa Makongoro pia ameipongeza Mahakama Kanda ya Sumbawanga kwa utendaji kazi wake mzuri, akisema umechangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi mkoani hapa.

Mahakama ya Tanzania huadhimisha Siku ya Sheria Nchini kila Mwaka, ambapo siku hiyo huashiria mwanzo rasmi wa Mwaka wa shughuli za Mahakama Tanzania. Ni siku muhimu ya kutathmini utendaji wa Mahakama na kuweka mwelekeo wa utoaji haki kwa Mwaka mzima.

Maadhimisho ya Siku ya Sheria Tanzania kwa Mwaka 2026 yanaongozwa na kauli mbiu isemayo “Mchango wa Mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa”, kauli mbiu inayolenga kuhimiza uwajibikaji, ufanisi na ushirikishwaji wa wananchi katika mfumo wa utoaji haki nchini.