Wadau wa Elimu katika Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga leo Februari 10, 2026 wameketi kikaoni kujadili masuala mbalimbali ya elimu katika shule za Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa lengo la kuimarisha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji.

Kikao kilichowaleta pamoja Wataalam wa Mkoa, Halmashauri, Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga, Watendaji wa Kata, Maafisa Elimu, Wakuu wa Shule, Walimu Wakuu pamoja na Wazee Mashuhuri wa Mkoa wa Rukwa.

Kupitia kikao hicho kilichoongozwa na Mwenyekiti wake, Mkuu wa Wilaya ya Sumbawanga Mhe. Nyakia Ally Chirukile amesisitiza uzalendo wa ufundishaji kwa Walimu wa shule za Sekondari na Msingi ili kuinua ufaulu kwa Wanafunzi na kudumisha matokeo chanya yanayopatikana katika Manispaa ya Sumbawanga.

Katika kikao hicho, Mhe. Chirukile ameipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga kwa kuongoza Mkoa wa Rukwa katika ufaulu wa Mtihani wa Kidato cha Nne 2025 na Mkoa wa Rukwa kuwa nafasi ya Tisa Kitaifa katika Mtihani wa Kidato cha Nne 2025, akieleza kuwa mafanikio hayo ni matokeo ya mshikamano wa Serikali, wadau wa elimu, juhudi za Walimu pamoja na usimamizi thabiti wa Sekta ya Elimu ndani ya Manispaa na kusisitiza kuwa elimu ipewe kipaumbele kuanzia sasa.

Mhe. Chirukile ameongeza kuwa ushirikiano baina ya Serikali, Viongozi wa Siasa pamoja na Wazee mashuhuri na wa Mila ni muhimu katika kuongeza msukumo juu ya uelewa wa Jamii kuzingatia elimu kwa kupeleka watoto shule na kusimamia maendeleo ya Wanafunzi.

Pamoja na hayo Mhe. Chirukile amesema kuwa Watoto wakipelekwa shule itaondoa wimbi la Watoto Mitaani ambao watapata ujuzi utakaosaidia maarifa kwa maendeleo endelevu.

Katika hatua nyingine, Mhe. Chirukile amesema kuwa Serikali inaendelea kuwekeza miundombinu bora ya elimu, vifaa vya kufundishia, Walimu pamoja na lishe shuleni, hali ambayo kwa sasa imeendelea kuimarika kila siku na kuchangia matokeo chanya katika Sekta ya Elimu.