Mwenyekiti wa
Tume ya Utumishi wa Umma nchini (PSC), Jaji (Mst.) Hamisa Kalombola,
ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia
Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiwezesha Tume kifedha, hali inayowezesha
utekelezaji wa majukumu yake ikiwemo kuendesha vikao na kutoa mafunzo
mbalimbali kwa watumishi wa umma.
Jaji Kalombola ameyasema hayo,
wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha Tume ya Utumishi wa Umma wa Mamlaka
za Maji nchini, kinachoendelea mjini Morogoro, kikilenga kujadili
utekelezaji wa Sheria ya Utumishi wa Umma Sura ya 298, pamoja na
matumizi ya mfumo wa kielektroniki wa kushughulikia rufaa na malalamiko,
sambamba na uwasilishaji wa taarifa za kiutumishi kwa Tume.
Amesema
kuwa, uwezeshaji huo wa kifedha umeiwezesha Tume kutekeleza majukumu
yake kwa ufanisi zaidi, hali inayochangia kuboresha usimamizi wa
utumishi wa umma na kuinua ubora wa huduma zinazotolewa kwa wananchi.
Aidha
Jaji Kalombola amesema kuwa, kupitia vikao na mikutano mbalimbali ya
kushughulikia rufaa na malalamiko ya watumishi wa umma, Tume imebaini
kuwepo kwa ukiukwaji wa sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma
katika baadhi ya Mamlaka za Majisafi na Usimamizi wa Mazingira nchini,
hali iliyoibua umuhimu wa kuitisha kikao kazi hicho.
“Tume
imekuwa ikikumbana na changamoto hizi kwa muda mrefu, hivyo tukaona kuna
umuhimu wa kukutana ili kujadili kwa pamoja namna ya kurekebisha hali
hiyo na kusukuma mbele maendeleo ya taifa,” amesema Jaji Kalombola.
Ameongeza
kuwa, ukiukwaji wa taratibu hizo husababisha baadhi ya rufaa kurejeshwa
ili kusikilizwa upya, jambo linalochelewesha haki na mambo mengi ya
watumishi wa umma.
Kwa upande wake, Kaimu Katibu wa Tume ya
Utumishi wa Umma John Mbisso amesema kuwa, lengo la kikao kazi hicho ni
kutoa mafunzo kuhusu Sheria ya Utumishi wa Umma na utekelezaji wake,
kufuatia kubainika kwa ukiukwaji wa sheria hizo katika taasisi
mbalimbali.
Amesema Tume imeandaa mfumo wa kielektroniki kwa
ajili ya kushughulikia rufaa na malalamiko, hivyo kikao hicho
kimewakutanisha Wakurugenzi wa Usimamizi wa Rasilimali Watu na Utawala,
Wakurugenzi wa Huduma za Sheria pamoja na Wakuu wa Vitengo vya TEHAMA
kutoka Mamlaka za Maji ili kuujadili na kuuelewa mfumo huo
Tunapatikana Kupitia