Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba, ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Amali ya Mkoa wa Rukwa inayojengwa katika Kata ya Majengo, wilayani Nkasi, leo Machi 9, 2026.
 
Shule hiyo ya amali inayotoa mafunzo ya ufundi inajengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.6 na katika awamu ya kwanza inatarajiwa kuwa na jumla ya majengo 19, yakiwemo jengo la utawala, madarasa, maabara, karakana za mafunzo, bwalo la wanafunzi pamoja na vyoo.
 
Kwa mujibu wa taarifa ya mradi, hadi sasa ujenzi wa madarasa nane pamoja na jengo la utawala umekamilika na miundombinu hiyo tayari imeanza kutumika. Aidha, ujenzi wa jengo la TEHAMA na maktaba, nyumba ya mtumishi pamoja na vyoo vya wavulana na wasichana pia umekamilika na majengo hayo yanaendelea kutoa huduma.
 
Ujenzi wa miundombinu mingine unaendelea katika hatua mbalimbali, ikiwemo karakana ya uashi iliyo katika hatua ya ufungaji wa mfumo wa umeme, karakana ya ufundi magari na mitambo iliyo katika hatua ya uwekaji wa sakafu na ufungaji wa umeme, pamoja na mabweni manne ambapo matatu yako katika hatua ya uwekaji wa dari na moja katika hatua ya uwekaji wa sakafu na dari.
 
Mradi huo unatarajiwa kuongeza fursa za mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana wa Mkoa wa Rukwa na maeneo jirani, hatua itakayowawezesha kujiajiri na kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya mkoa na Taifa kwa ujumla.
 
Waziri Mkuu yuko mkoani Rukwa katika siku ya pili ya ziara yake ya kikazi ya siku tatu iliyoanza Machi 8, 2026.