Katika juhudi za kukabiliana na vitendo vya kilimo haramu vinavyoathiri usalama
na ustawi wa jamii, mamlaka wilayani Butiama mkoani Mara zimeendesha operesheni
maalum katika Kijiji cha Mirwa, Kata ya Mirwa, eneo linalopakana na mgodi wa
Buhemba. Operesheni hiyo imelenga kubaini na kuchukua hatua dhidi ya shughuli
za kilimo cha bangi zilizokuwa zikifanyika kwa siri.
Akiwasili katika eneo la tukio, Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Thecla Mkuchika
alionesha kusikitishwa na uwepo wa kilimo hicho haramu na kutoa onyo kali kwa
wanaojihusisha nacho.
Aidha, alielekeza Jeshi la Polisi kuendeleza operesheni kama hizo ili kuwabaini
na kuwaondoa kabisa wahusika katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo.
Katika operesheni hiyo, zaidi ya hekari tatu za mashamba ya bangi ziligunduliwa
na kuteketezwa kwa moto, pamoja na zaidi ya magunia sita ya bangi iliyokuwa
tayari imehifadhiwa kwa ajili ya kusafirishwa na kuingizwa katika matumizi.
Jeshi la Polisi pia lilifanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja aliyekutwa
akijihusisha na kilimo hicho katika makazi yake, ambapo ilielezwa kuwa baadhi
ya mashamba yalikuwa yamechanganywa na mazao halali kama mahindi na ufuta kwa
lengo la kuficha shughuli hiyo haramu.
Baada ya kushuhudia hali hiyo, Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Butiama, Fredi Mmasi
alielekeza mashamba yote yaliyobainika kuteketezwa mara moja, huku mtuhumiwa
akidai kuwa hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kujihusisha na kilimo hicho na
hakutoa majibu ya moja kwa moja alipoulizwa kuhusu ushirikiano na watu wengine.
Akizungumza katika eneo la tukio, kaka wa mtuhumiwa, Chacha Itundura, alisema
kuwa mara kadhaa amekuwa akimshauri ndugu yake kuacha kilimo hicho, huku
mtuhumiwa akidai kuwa analima kwa mara ya mwisho kabla ya kuacha baada ya
mavuno.
Operesheni hiyo ni sehemu ya jitihada za Jeshi la polisi zinazoendelea za
kulinda jamii dhidi ya athari za dawa za kulevya na kuhakikisha sheria
zinafuatwa.
Tunapatikana Kupitia